"Kumalizika kwa mradi wa SWIL isiwe sababu ya kubweteka kuzifanyia kazi changamoto za kijamii-CB" DC Chake Chake.
Imeandikwa na Hassan Msellem, Pemba.
Mkuu wa Wilaya ya Chake Chake Ndugu Abdalla Rashid Ali, amewataka Wahamasishaji Jamii (CB) Kisiwani Pemba ambao walikuwa wadau wakubwa katika utekelezaji wa Mradi wa uhamasishaji Wanawake katika Uongozi (SWIL) kuendelea kuzifanyia kazi changamoto zinazowakabili Wananchi ili ziweze kupatiwa ufumbuzi.
Mkuu huyo wa Wilaya ametoa kauli hiyo huko katika ukumbi wa Maktaba Chake Chake wakati alipokuwa akifunga huo wa miaka minne, amesema kumalizika kwa mradi huo kumeweza kusaidia kwa kiasi kikubwa katika utatuzi wa changamoto mbali mbali za Kijamii na Uongozi kwa Wanawake.
Mratibu wa Jumuiya ya Utetezi wa kijinsi na mazingira Pemba (PEGAO) Bi. Dina Juma Makota amesema kupitia mradi huo wamefanikiwa kuwafikia Wananchi 6,894 idadi ambayo imepindua shebaha ya mradi huo kwa upande wa Kisiwa cha Unguja na Pemba ambayo ni kuwafikia Wananchi 6000 kwa kipindi cha miaka 4 ya utekelezaji wake.
Kwa upande wake Mratibu wa Tamwa Pemba Bi. Fat-hiya Mussa Said, amesema kupitia Mradi wa SWIL wamefanikiwa kutatua changamoto mbali mbali za Kijamii ikiwemo idadi ya Wanawake wenye elimu ya Uongozi, kujua kusoma na kuandika, kuondoka idado ya madarasa katika Skuli mbali mbali, matundu ya vyoo pamoja akina baba ambao wametoa ruhusa kwa wake zao kujiingiza katika vyama vya siasa na kugombea nafasi mbali mbali za Uongozi.
Hamad Omar Khamis CB Wete, ametoa shukrani kwa taasisi mbali mbali za Serikali ikiwemo Ofisi za Wakuu wa Wilaya kwa ushirikiano na Wahamasishaji Jamii katika utekelezaji wa Mradi huo.





Comments
Post a Comment